MAANDALIZI ya kuwalipa fidia wakazi wa Mbagala walioathiriwa na mabomu yameingia dosari baada ya baadhi ya majina ya watu kukosekana kwenye orodha ya malipo, huku majina mengine yakitofautiana na namba za nyumba zilizoathiriwa.
Jumla ya Sh8.5 bilioni zimetengwa kwa ajili ya malipo ya fidia kwa wakazi ambao nyumba zao ziliathiriwa na milipuko ya mabomu iliyotokea Aprili 29 kwenye ghala la silaha la kambi ya Jeshi la Wananchi (JWTZ) iliyo Mbagala na kusababisha vifo vya zaidi ya watu 29.
Fedha hizo zitatumika kulipa fidia nyumba 9,259 zilizoharibiwa na mabomu hayo na ambazo zilihakikiwa na serikali.
Lakini uchunguzi wa gazeti hili jana umebaini kuwa mchakato wa malipo hayo umeanza kuingia dosari baada ya watu kadhaa waliofika ofisi ya afisa mtendaji kata ya Mbagala Kuu, kugundua kuwa majina yao hayapo kwenye orodha iliyobandikwa ukutani na wengine kukuta tofauti ya majina na namba za nyumba.
Afisa mtendaji wa kata hiyo, Basil David alisema kuwa zaidi ya watu 50 waliofika ofisini kwake kuangalia majina yao, walikuta aidha yamekosewa au hayaendani na namba za nyumba zao.
"Ni kweli zimejitokeza kasoro kwenye mchakato huu. Zipo namba za nyumba zilizokosewa na majina mengine yanatofautiana na namba za nyumba hizo,” alisema.
"Kutokana na hali hii tumeziagiza ofisi za serikali za mitaa kuorodhesha majina ya watu ambao majina yao au namba zao zimekosewa, ili ayapeleke kwa mkuu wa mkoa kwa ajili ya kufanyiwa marekebisho kabla ya kuandaliwa kwa hundi za malipo," alisema.